Mjumbe
 wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za mitaa (LAAC) za Mitaa, 
Kangi Lugola akizungumza wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichofanyika 
Dar es Salaam jana. Kushoto ni Mjumbe mwenzake, Omari Nundu.
 Licha
 ya Bunge kuazimia kuwa wenyeviti wa kamati zake waliotajwa kuhusika 
kwenye kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow wavuliwe nyadhifa zao, hali 
imekuwa tofauti katika vikao vya kamati hizo vilivyoanza jana baada ya 
baadhi yao kuongoza vikao hivyo. Jana, Kamati Kuu ya CCM imeamua 
viongozi hao, Andrew Chenge, William Ngeleja Na Profesa Anna Tibaijuka 
wafikishwe Kamati ya Maadili ya chama.
Awali,
 walitakiwa kuachia ngazi na kamati zao katika mabano ni Ngeleja 
(Katiba, Sheria na Utawala), Chenge (Bajeti) na Victor Mwambalaswa 
(Nishati na Madini).
Kikao
 cha 16 na 17 cha Bunge kiliazimia kuwa kamati husika za kudumu za Bunge
 zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya Mkutano wa 18 wa
 Bunge unaoanza Januari 27, kuwavua nyadhifa zao wenyeviti tajwa wa 
kamati husika.
Hata hivyo, jana, Ngeleja alisema anaendelea na madaraka yake, kwa kuwa hatua iliyopo sasa ni ya uchunguzi.
“Mimi
 naendelea na kazi zangu kama mwenyekiti wa kamati, najua uchunguzi wa 
suala hili bado unaendelea, baada ya hapo ikithibitika ndipo Bunge 
litachukua uamuzi nami sitakuwa na budi kutekeleza,” alisema Ngeleja.
Aliongeza: “Ingawa ninajua kuna shinikizo kwa baadhi ya watu kwa sababu wanazozijua wao hawapendi kutuona katika nafasi hizi.”
Kwa
 upande wake, Chenge alisema: “Sikuwahi kutangaza kujiondoa katika 
nafasi hii ya uenyekiti. Nimeshangaa taarifa zilizotolewa katika baadhi 
ya vyombo vya habari.”
Alisema
 tuhuma zinazomkabili hazimuumizi kichwa kwa sababu hazina ukweli, 
“Dhamira hainiumi kwa sababu siwezi kushiriki kuiba fedha za wananchi. 
Mimi ni kama tumbili hata hapa nitaruka.”
Makamu
 mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk Festus Limbu alisema suala la Chenge 
linasubiri uamuzi utakaotolewa na Spika wa Bunge, Anne Makinda. “Kamati 
imeamua kwa busara Chenge akae pembeni na makamu mwenyekiti aongoze 
vikao huku ikisubiri hatua atakazozichukua Spika (Makinda)...lakini siyo
 taarifa kwamba Chenge kajiuzulu, siyo kweli.”
“Unajua
 suala hili unaweza kusema bado ni bichi, Chenge ni mwenyekiti mteule wa
 Spika, lakini wenyeviti wengine wanachaguliwa na wajumbe wa kamati zao,
 labda Spika hajaona wa kumteua au anataka kuiachia kamati ifanye 
uchaguzi, hili litategemea na yeye,” alisema Limbu ambaye ni Mbunge wa 
Magu (CCM)
Kuhusu
 wafadhili wa maendeleo ambao kamati hiyo ilikutana nao jana alisema 
wametoa asilimia 50 ya Dola 558 milioni ambazo wahisani hao waliahidi.
Kikao
 cha Kamati ya Nishati na Madini kiliongozwa na Makamu mwenyekiti wake, 
Jerome Bwanausi ambaye alilithibitishia gazeti hili kwamba hawakufanya 
uchaguzi wowote.
Alipotafutwa kwa simu Mwabalaswa na kutakiwa kuzungumzia hatima yake, alijibu kuwa hawezi kuzungumzia suala hilo kwenye simu.
Mkurugenzi
 wa Idara ya Shughuli za Bunge, John Joel alisema: “Suala halipo 
kikanuni, bali ni maagizo yaliyotolewa na Bunge kwa hiyo mwenye nafasi 
nzuri ya kulizungumzia ni Spika.”
Hata
 hivyo, habari zilizopatikana jana usiku ndani ya Kamati Kuu ya CCM 
zilieleza kuwa, Ngeleja, Chenge pamoja na Profesa Tibaijuka suala lao 
imeachiwa Kamati ya Maadili ya CCM chini ya mwenyekiti wake, Philip 
Mangula.
LAAC yalishukia jiji
Katika
 hatua nyingine, Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), 
imeitaka Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam leo itoe taarifa za 
kueleweka kuhusu uuzaji wa hisa zake na mikataba kwa Kampuni ya Simon 
Group. Uamuzi huo umekuja baada ya Mkurugenzi wa jiji hilo, Wilson Kabwe
 na Meya, Dk Didas Masaburi kujichanganya wakati wakijibu maswali ya 
uuzaji wa hisa hizo kwa kampuni hiyo ambayo inamiliki Shirika la Usafiri
 Dar es Salaam (UDA).
Mwenyekiti
 wa LAAC, Rajab Mbarouk Mohammed alitoa maazimio hayo baada ya kuibuka 
mvutano kati ya wajumbe wa kamati hiyo na Dk Masaburi na Kabwe kuhusu 
uuzwaji wa hisa hizo ambazo ni asilimia 21.
Mvutano
 uliibuka baada ya Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola kueleza kuwa mmiliki 
wa Simons Group, Robert Kisena alitaka kununua hisa hizo, lakini jiji 
lilikataa.
Kwa
 upande wake, Kabwe alikiri kuwa walikataa zisinunuliwe kwa sababu 
alikuwa na shaka kama Simon Group ingeweza kulipa fedha zote kama 
unavyoeleza mkataba. Hisa hizo zinauzwa kwa Sh5 bilioni.
Kitendo
 cha wajumbe wa kamati hiyo kulichachamalia zaidi suala hilo ambalo 
liliwagawa katika Bunge la Bajeti kinatafsiriwa kuwa ni kutaka kulipa 
kisasi baada ya Dk Masaburi wakati akitoa ufafanuzi kuhusu UDA, Mei 
mwaka jana katika kikao cha Bajeti, kutumia lugha ya kuudhi kwa wabunge.
Pia,
 kamati ilihoji kwa nini Jiji la Dar es Salaam lisivunjwe na kuwa na 
kitengo kidogo kutokana na kutokuwa na majukumu ya moja kwa moja kwa 
wananchi.
Hoja
 hiyo iliibuliwa na Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige kwamba kuna 
haja ya kuvunjwa kwa jiji hilo na badala yake kubakiwe watu wachache 
(meya, mkurugenzi na katibu muhtasi) ambao watashungulika na masuala 
mtambuka.
Alisema
 pia kuna haja ya kuangalia upya, sheria ambayo inaipa mamlaka 
halmashauri ya jiji kukusanya ushuru wa maegesho ili kazi hiyo ifanywe 
na manispaa za jiji hilo na kisha kutoa gawiwo kwa jiji.
Katika
 ziara ya LAAC iliyofanya katika manispaa za jiji hilo hivi karibuni, 
ilipokea malalamiko ya kutopewa fedha za maegesho kutoka jiji, jambo 
linalozikwamisha kufanya shughuli za maendeleo. Manispaa zote tatu, 
Ilala, Kinondoni na Temeke zinatakiwa kugawana asilimia 75 ya mapato ya 
maegesho na asilimia 25 inabaki jiji.
Akijibu
 hoja ya ushuru, Dk Masaburi alisema madai hayo huenda yakawa na ukweli 
na kuwa tatizo lililopo ni mkataba uliokuwa umeingiwa na wakala, Nation 
Park Solution (NPS).
Awali,
 Mbarouk aliupa uongozi wa jiji siku 19 kuanzia leo kuhakikisha 
inapeleka ripoti ya tathmini ya mali kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa 
Hesabu za Serikali (CAG) kutokana na kushindwa kuikamilisha kwa miaka 
mitatu tangu kutolewa kwa agizo hilo.
PAC yataka uchunguzi NBC
Nayo
 Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imemwagiza 
Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru kuteua mkaguzi binafsi kwa ajili ya 
kufanya uchunguzi wa sababu za kushuka kwa mtaji wa Benki ya NBC ambayo 
inadaiwa Sh22.5 bilioni na Kampuni ya Absa Group Limited ya Afrika 
Kusini.
Mwenyekiti
 wa PAC, Zitto Kabwe alitaja maeneo yaliyosababisha mtaji kushuka kuwa 
ni mikopo iliyotolewa kwenye sekta ya usafirishaji, utekelezaji wa sera 
za Benki mama ya ABCA na mfumo wa uhasibu uliotambua mapato hewa. Iwapo 
Serikali itashindwa kulipa deni hilo hadi Machi mwaka huu, itapoteza 
asilimia 30 ya hisa zake katika NBC na hivyo benki hiyo kuwa chini ya 
Kampuni ya Absa ambayo ina asilimia 55 ya hisa za NBC.
Awali,
 kampuni hiyo ilikuwa na hisa asilimia 70 za benki hiyo lakini ikauza 
asilimia 15 ya hisa zake kwa Shirika la Fedha la Kimataifa.
Serikali
 ilikopa kiasi hicho cha fedha ili kutekeleza agizo la Benki Kuu ya 
Tanzania (BoT) ambayo mwaka 2012 iliiagiza NBC kuongeza mtaji wa 
biashara wenye thamani ya Sh75 bilioni, baada ya ule wa awali kushuka 
kwa asilimia 12.
Baada
 ya NBC kubinafsishwa mwaka 1997, Serikali ilibaki na asilimia 30 ya 
hisa na Kampuni ya Absa kuchukua asilimia 70, mtaji wa NBC ulishuka kati
 ya mwaka 2010 hadi 2012 baada ya benki hiyo kutoa mikopo ya magari wa 
Sh55 bilioni.
Baada
 ya mtaji wa NBC kushuka kwa asilimia 12, Benki Kuu Tanzania (BoT), 
iliagiza wanahisa wote watatu kuongeza mtaji. Kwa kuwa Serikali haikuwa 
na fedha za kuongeza katika mtaji, ilikopa Sh22.5 bilioni kwa Absa na 
kuzitoa kama mtaji kwa makubaliano ya kurejesha deni hilo ndani ya miaka
 miwili. Kuhusu taasisi ya mikopo ya Pride, Msajili wa Hazina alisema 
baada ya ukaguzi wa CAG walibaini kuwa taasisi hiyo iliondolewa kimakosa
 katika orodha ya taasisi za umma.
Alisema
 kutokana na hali hiyo kuna hasara ambayo serikali imeipata na 
kusisitiza kuwa watapokea taarifa rasmi ya uchunguzi wa taasisi hiyo 
uliofanywa na CAG na wataiwasilisha katika vikao vya Bunge vinavyoanza 
Januari 27.
Imeandaliwa na Fidelis Butahe, Ibrahim Yamola na Beatrice Moses.
USISITE KUTUACHIA UJUMBE WAKO HAPO CHINI 
 
 
 
.jpg) 
 
 
 
 
Post a Comment